Pages

Saturday, May 18, 2013

PENSHENI KWA WAZEE "NDOTO"

 

Rais Jakaya Kikwete akipewa maelezo na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma (PSPF), Adam Mayingu (kulia) alipotembelea banda la mfuko huko wakati wa ufungaji wa maonyesha ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, mjini Dodoma jana. Picha na Edwin Mjwahuzi 

 

Sakata la kuanzishwa kwa malipo ya pensheni kwa wazee bado ni giza nene baada ya Rais Jakaya Kikwete kutaka hatua hiyo isifanywe kwa kukurupuka.

Aidha, ameahidi kwamba Serikali italipa kiasi cha Sh6 trilioni inazodaiwa na Mfuko wa Hifadi wa PSPF.

Akizungumza jana wakati wa kilele cha Siku ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii katika Viwanja vya Mwalimu Nyerere Mjini Dodoma, Rais Kikwete alisema:

“Nakuagiza Waziri Kabaka, kuwa anzeni sasa kufikiria namna ya kuwalipa wazee pensheni, lakini msikurupuke kufanya hivyo kwani ni lazima kujiridhisha kwanza kabla ya kuanza kutoa mafao hayo maana mtaaibika.”

Aliongeza: “Nawaomba msiahidi kwa watu kitu msichoweza kukifanya na kuwa endelevu kwani mtaaibika, hivyo jipangeni vizuri kabla ya kuanza kutoa, waelezeni ukweli wazee.”

Rais aliwataka wataalamu kujifunza kutoka kwa nchi nyingine zilizofanikiwa akieleza kuwa wazee hawakuwahi kuchangia, hivyo kutoa malipo kwa wazee ambao ni zaidi ya milioni mbili nchini ni kazi kubwa.

Kwa upande mwingine Rais aliwatoa wasiwasi Watanzania kuwa mifuko ya hifadhi haitafilisika, huku akiahidi kuwa Serikali italipa deni lote inalodaiwa na mifuko ya hifadhi ya jamii ili kuhakikisha inafanya kazi yao iliyokusudiwa ikiwemo kuwalipa wastaafu.,

“Si kweli kuwa mfuko wa PSPF una hali mbaya kiasi cha kushindwa kujiendesha na kuitwa mahututi, bali mfuko huo unaidai Serikali kiasi cha fedha Sh6 trilioni na fedha hizo zitalipwa,”alisema Kikwete.

Alirudia ahadi yake kuwa Serikali italipa deni hilo na lile la Sh10 bilioni ambalo LAPF inaidai ili Serikali isiwatapeli wafanyakazi.



No comments:

Post a Comment