Pages

Tuesday, May 7, 2013

DRC eneo baya zaidi kwa mama kulea watoto

 

Wanawake katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo wakiandamana

 

Shirika la Save the Children, limeeleza kuwa, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kuwa ndio nchi ngumu zaidi duniani kulea watoto.

 

Nchi ya Finland imetajwa kuwa sehemu bora duniani kuwa mama, huku Sweden na Norway zikifuatia katika nafasi ya pili na tatu.

Shirika hilo la hisani limetumia vigezo vya huduma ya afya kwa akina mama, vifo vya watoto, elimu na kipato katika nchi 186 duniani kutoa takwimu hizo.

Nchini India, zaidi ya watoto 300,000 hufariki dunia saa 24 baada ya kuzaliwa, hivyo kuchangia 29% ya vifo vya watoto wanaozaliwa duniani kote imeeleza ripoti ya shirika hilo.

Nchi kumi zilizoshika nafasi ya mwisho zote zinatoka eneo la Kusini mwa Jangwa la Sahara, ambako kwa wastani, mwanamke mmoja katika 30 hufariki dunia kutokana na matatizo ya ujauzito na mtoto mmoja kati ya saba hufariki kabla ama baada ya kufikisha umri wa miaka mitano.

Nchini DRC, vita na umasikini vimewaacha akina mama wakiwa dhoofu kiafya na bila msaada wowote hasa wakati wa hatari kubwa katika maisha yao.

Nchi nyingine zilizotajwa kuwa hatari ni Somalia, Sierra Leone, mali, Niger, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Gambia, Nigeria, Chad na Cote D’Ivoire.

Shirika hilo la hisani limesema, ukosefu wa lishe bora ni sababu kubwa ya kuongezeka kwa idadi ya vifo vya akina mama na watoto wachanga katika nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara, huku 10% - 20% ya akina mama wakiwa hawana uzito unaostahili.

Kinyume chake, matokeo hayo yanaonesha kuwa, Finland ni nchi bora kuwa mama, huku hatari za vifo vitokanavyo na ujauzito ikiwa ni moja kati ya akina mama 12,200 na watoto katika nchi hiyo wakihudhuria karibu miaka yote 17 ya elimu ya awali.

Congo ni mahali hatari zaidi kwa akina mama

Sweden, Norway, Iceland na Uholanzi zilikuwa pia miongoni mwa nchi bora 10, ambapo Marekani iko nyuma katika nafasi ya 30.

Lakini jambo la kustaajabisha, ripoti ya shirika hilo imebaini kuwa, Marekani ina kiwango cha juu cha vifo vya watoto wanaozaliwa katika nchi zenye viwanda duniani, ambapo watoto 11,300 hufariki dunia katika siku wanayozaliwa kila mwaka.

Shirika hilo limesema, hali hiyo inasababishwa na idadi kubwa ya watu nchini Marekani pamoja na wingi wa watoto wanaozaliwa kabla ya wakati. Marekani ni miongoni mwa nchi zenye kiwango cha juu cha watoto wanaozaliwa kabla ya wakati ikiwa na uwiano wa mtoto mmoja kati ya wanane.

Ipoti hiyo imegundua kuwa, akina mama na watoto hufariki dunia kwa idadi kubwa huko Kusini mwa Asia kuliko eneo lolote duniani, ikikadiriwa kuwa, watoto 423,000 hufariki dunia siku wanayozaliwa kila mwaka.

India imetajwa kuwa na idadi kubwa ya vifo vya watoto wachanga,(ikiwa ni 29% ya vifo duniani) na pia vifo vingi vya akina mama kuliko nchi yoyote duniani ambapo akina mama 56,000 hufariki kila mwaka.

No comments:

Post a Comment