Pages

Tuesday, May 7, 2013

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU TUKIO LA MLIPUKO KANISANI ARUSHA

 

 


 

 

 TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ametuma salaam za pole na rambirambi kwa waumini wa Kanisa Katoliki nchini na Watanzania wote kwa ujumla kutokana na mlipuko uliotokea katika Kanisa la Olasiti, Jijini Arusha, uliosababisha vifo na majeruhi, huku wengine wakipatwa na mshtuko mkubwa kutokana na tukio hilo.


 

Mwenyekiti Mbowe ametoa salaam hizo alipozungumza kwa njia ya simu na Katibu wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), Padri Antony Makundi, jioni ya Jumapili, baada ya kupata taarifa za tukio la mlipuko huo unaodhaniwa kuwa ni bomu.


 

"Tumepokea habari za tukio la mlipuko uliotokea leo (jana) katika Kanisa la Olasiti huko Arusha kwa mshtuko na masikitiko makubwa. Kupitia kwako tunapenda kutoa pole kwa familia, ndugu, jamaa na waumini wa Kanisa la Olasiti waliopatwa na msiba, waliojeruhiwa na wengine waliopatwa na mshtuko mkubwa kutokana na tukio hilo lisilokuwa la kawaida.


 

"Tunapenda pia kupitia salaam hizi, kuwapatia pole waumini wote wa Kanisa Katoliki nchini na Watanzania wote walioguswa na tukio hili la leo (jana). Mwenyezi Mungu awajaze imani, nguvu na kuwapatia moyo wa subira nyote, wakati huu mgumu wa majonzi mazito na kutafakari tukio hilo.


 

"Tumuombe awajalie uponyaji wa haraka na ahueni na afya njema wale wote waliojeruhiwa na waliopatwa na mshtuko kutokana na tukio hilo. Kupitia kwako pia naomba utufikishie salaam zetu za pole za uongozi kwa Rais wa TEC, Askofu Tarcisius Ngalalemkutwa kwa niaba ya uongozi wa Kanisa Katoliki nchini," alisema Mwenyekiti Mbowe.


 

Mwenyekiti Mbowe, ambaye pia ni Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni (KUB) aliwataka Watanzania wote kuwa watulivu wakati huu, wakati ambapo serikali kupitia vyombo vya dola inafanya uchunguzi wa tukio hilo. Alisema serikali haina budi kuchunguza na kutoa taarifa za matukio mengine yote ya namna hiyo ili kuwahakikishia Watanzania wote haki na matumaini ya kuendelea kuishi kwa utulivu katika nchi yao.


 


 

Imetolewa Mei 6, 2013,Dar es Salaam na;


 

Kurugenzi ya Habari na Uenezi

Makao Makuu ya CHADEMA.

No comments:

Post a Comment