Pages

Sunday, May 12, 2013

HUJUMA:MAFUTA YA KULA YAINGIZWA NCHINI BILA KODI


TRA

TRA: Tukielekezwa tutafanya uchunguzi

 

TBS: Tupeni muda, tutaongea jumanne

 

Kashfa ya ukwepaji kodi na uingizaji bidhaa zinazosadikiwa kuwa bandia, imeibuka wakati bidhaa hizo zikipitishwa katika `bandari bubu’ iliyopo kwenye ufukwe wa Mbweni jijini Dar es Salaam, NIPASHE Jumapili limebaini.
Hali hiyo inayohujumu uchumi wa taifa, inafanyika huku jiji hilo likiwa Makao Makuu ya vyombo vya dola vyenye mamlaka na majukumu tofauti, yanayoweza kuudhibiti uovu huo.

Uchunguzi wa NIPASHE Jumapili umebaini kuwa shehena za bidhaa mbalimbali yakiwamo mafuta ya kula, zinaingizwa bila kificho kwenye `bandari’ hiyo, kisha kusafirishwa maeneo tofauti ya nchi. Kwa hali hiyo, `bandari bubu’ isiyokuwa na udhibiti wa aina yoyote, imekuwa moja ya vituo vikuu vya kukwepa kodi na uingizaji wa bidhaa `feki’.

Licha ya hujuma hizo, bidhaa zinazopitia katika eneo zikitokea nje ya nchi, zimekuwa kichocheo cha ‘kuua’ bidhaa za ndani, kutokana na kutolipiwa kodi na ushuru, hivyo kuuzwa kwa bei rahisi zaidi. “Unaponunua bidhaa zilizopitishwa Mbweni, gharama yake ni ndogo hivyo inakuwa rahisi kulimiliki soko la ndani na kuua ushindani,” kilieleza moja ya vyanzo vyetu.

Miongoni mwa bidhaa za ndani zilizoathirika kutokana na kuwepo kwa `bandari bubu’ hiyo ni mafuta ya kula yanayozalishwa nchini. Uchunguzi zaidi ulibaini kuwa, shehena za mafuta ya kula kutoka nje, zimekuwa zikishushwa kisiwani Unguja na kuingizwa Tanzania Bara kwa majahazi yenye uwezo wa kubeba ‘madumu’ 500, kisha kupakuliwa katika `bandari bubu’ ya Mbweni.

Ingawa haikujulikana ikiwa waingizaji wa bidhaa hizo ni wafanyabiashara halali ama wafanya magendo, lakini baadhi ya mafuta ya kula ambayo nembo zake zilionekana ni Oki, Asma, Partner, Viking na Premier Gold kutoka Malasyia. Mafuta hayo yanapofika sokoni, yanauzwa kwa kati ya Shilingi 38,0000 hadi 45,000 kwa ujazo wa lita 20, wakati bei ya mafuta ya kula yanayotengenezwa nchini kwa ujazo huo ni kati ya Shilingi 52,000 na 55,0000.

Baadhi ya wafanyabiashara  katika eneo la Mbweni, walithibitisha kuwepo hujuma ya ununuzi wa bidhaa hizo, licha ya kuwepo msako unaofanywa mara chache na Mamlaka ya Mapato nchini (TRA). Walisema, TRA inafanya msako hadi majini, lakini kutokana na mazingira yanayoashiria rushwa, ushushaji wa shehena hizo umekuwa ukiendelea.

"Unajua hela ni kila kitu, TRA wanawakamata wahusika, wakipewa hongo hawachukui hatua yoyote… wafanyabiashara wengi wanaingiza bidhaa nyingi kupitia hapa na si mafuta ya kula tu," kilieleza chanzo hicho. Mmoja wa wafanyabiashara wa Tegeta jijini Dar es Salaam, John Massawe, anathibitisha kuwepo bidhaa yakiwamo mafuta ya kula, zinazouzwa kwa ‘bei chee’ kutokea Mbweni.

Anasema gharama ndogo za ununuzi wa `mafuta ya Mbweni’ zinamfanya awekeze katika kuyanunua na kuyauza, hivyo kupata faida kubwa. “Mafuta ya Tanzania yanachukua muda mrefu kutoka kwa sababu ya ukubwa wa bei yake ikilinganishwa na haya yanayotoka nje kupitia Mbweni,” alisema.

Zipo taarifa zinazowahusisha baadhi ya wafanyabiashara wakubwa katika uingizaji wa bidhaa na mafuta ya kula kupitia ‘bandari bubu’ hiyo. "Kwa sasa siagizi tena haya mafuta ya ndoo kwani yana hasara, ninanunua yanayotoka nje ya nchi kama Premier, yanauzika kwa haraka na sijapata malalamiko kama yana madhara," alisema

WAMILIKI WA VIANYA WAJA JUU

Baadhi ya wamiliki wa viwanda vya kuzalisha mafuta ya kula, wamelalamikia hujuma zinazofanyika kwenye bandari hiyo, kwamba zinawasababishia hasara. Christopher Mutayoba ni mmiliki wa kiwanda cha CRM Investment, anasema kushindwa kuidhibiti hujuma zinazofanywa kwenye ‘bandari bubu’ ya Mbweni, kunadidimiza viwanda vya wazawa na kuvifanya vishindwe kukua.

Mutayoba alisema serikali inapaswa kuchukua hatua kali zenye nia na utashi wa kuwatetea wazawa, ili waweze kulimiliki soko la ndani na kusafirisha bidhaa zao nje. "Ukiona tunafanya biashara ya mafuta ni mpaka yanayotoka nje yakosekane sokoni,” alisema.

Mmiliki mwingine wa kiwanda cha mafuta ya kula jijini ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini, amethibitisha bidhaa hiyo kukosa soko la ndani. vAlisema serikali inakusanya kodi kubwa kwa viwanda vya ndani, wakati bidhaa za nje zikiingizwa kinyemela bila kulipiwa kodi na ushuru.

Catherine John ni mkazi Kinondoni, alisema haelewi kama mafuta hayo yana madhara, lakini amekuwa akiyanunua kutokana na kuuzwa kwa bei rahisi. Baadhi ya vyombo vya kuhifadhiwa mafuta hayo vimebainika kuwa na nembo ya uthibitisho ya Shirika la Viwango (TBS) huku mengi yao yakiwa hayana.

Taarifa zinadai kuwepo ushindani mkali katika ununuzi wa mafuta hayo, kutokana na kuhitajiwa na wafanyabiashara wengi hasa wa rejareja.

Yanapopakuliwa, mafuta hayo yanasafirishwa kwa kutumia magari binafsi na wakati mwingine daladala. NIPASHE Jumapili ilishuhudia sehemu ya shehena iliyopakiwa kwenye daladala, ikishushwa eneo la Tegeta na kupakiwa kwenye garia aina ya Fuso iliyokuwa imeegeshwa kandoni mwa barabara.

Mkurugenzi wa Huduma na Elimu wa TRA, Richard Kayombo, alisema wanachohitaji ni kupata taarifa kamili kuhusu hujuma hiyo ili waishughulikie. "Ni kweli kuna bandari bubu, ila tunaomba utupatie taarifa kamili za huo mzigo ili tufahamu umeingizwaje, unamilikiwa na nani, aliyeuagiza na unashukia eneo lipi, ili tuwapatie maafisa wetu na polisi kwa uchunguzi," alisema

Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Viwanda na Biashara, Mahamoud Mgimwa, alisema hawana taarifa kuhusu hujuma hiyo. "Hata mimi nimeshangazwa, iweje mafuta hayo yanayotoka nje yauzwe rahisi kiasi hicho, huko nikuua viwanda vya ndani," alisema.

Mkurugenzi wa Uthibiti wa Ubora wa TBS, Tumain Mtitu, alisema hawana ‘data’ kamili na kwamba hawaijui kashfa hiyo. "Nifuate wiki ijayo kwa sasa nashindwa kuzungumzia kwa kuwa sina `data’ kamili, nitumie hayo majina ya hayo mafuta," alisema.

CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment