Pages

Thursday, May 16, 2013

Wanafunzi Lupata wachoma bweni



 

WANAFUNZI wa Shule ya Sekondari Lupata, inayomilikiwa na Jumuiya ya Wazazi (CCM) wilayani Rungwe wamefanya vurugu na kuliteketeza kwa moto bweni la wavulana wakipinga kitendo cha wanafunzi wenzao watatu kusimamishwa masomo kwa utovu wa nidhamu.

Taarifa za tukio hilo zimetolewa jana na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, Diwani Athuman, na kwamba vurugu hizo zilitokea juzi majira ya saa 2:00 usiku baada ya wanafunzi waliosimamishwa masomo kuwahamasisha wenzao kupinga adhabu hiyo.

Kamanda Diwani alisema tukio hilo limesababisha uharibifu mkubwa wa mali za shule hiyo ingawa moto huo haukusababisha madhara.

Alisema chanzo cha vurugu hizo ni kutokana na wafunzi hao; Joseph Robert (18) mwanafunzi wa kidato cha nne, Mwita Chacha (17) mwanafunzi wa kidato cha tatu wote wakazi wa Kitunda, Dar es Salaam kusimamishwa masomo kwa utovu wa nidhamu.

Alisema mwanafunzi mwingine anayehusika katika kuhamasisha wenzao kufanya vurugu hizo ni Daniel David (18) anayesoma kidato cha tatu na mkazi wa Ipinda, wilayani Kyela.

Kamanada huyo alisema bweni lililoteketea kwa moto lilikuwa na wanafunzi zaidi ya 50 ambao waligoma kuwaunga mkono wenzao.

Kutokana na tukio hilo, alisema wanafunzi 15 wakiwamo waliosimamishwa masomo wanashikiliwa na polisi kwa ajili ya mahojiano zaidi.

No comments:

Post a Comment